Monday, February 19, 2018

Hongera Waziri Mkuu kufanya ziara Mwanza

Antony Sollo  Misungwi

Ziara ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa Jijini Mwanza imekuwa ya mafanikio,hii ni baada ya kubaini mambo uozo lakini haya ni kwa uchache kutokana na siri kubwa iliyofichika kutokana uozo mwingi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Wilaya ya Misungwi Mkoani Mwanza.

Historia ya kuwepo kwa Uozo Misungwi.

Wilaya ya Misungwi ni moja kati ya Wilaya kongwe nchini ambazo zimekuwa zikiongoza kwa kupata hati chafu na imekuwa bahati kwa Mawaziri Wakuu wa awamu ya Nne na ya tano ambao wote wamebahatika kukumbana na uozo jambo lililopelekea kuwatumbua watumishi wachache wa Halmashauri hiyo huku vinara wakiachwa kutokana na kuwepo kwa mnyororo mkubwa ambao umetengenezwa maalumu kwa ajili ya upigaji dili.

Katika ziara yake hivi karibuni,Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Khassim Majaliwa amemsimamisha kazi Mwanasheria wa Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi,  Alphonce Sebukoto,  na kuagiza achungunzwe na vyombo husika.

Waziri Mkuu alifikia hatua hiyo baada Mwanasheria huyo kuonekana kushindwa kutekeleza majukumu yake ipasavyo ikiwa ni pamoja na kushindwa kuishauri vyema halmashauri hiyo na kuisababishia hasara ya sh. milioni 279.


Majaliwa alimsimamisha kazi Sebukoto 19februari mwaka huu wakati akizungumza na watumishi na madiwani wa halmashauri hiyo akiwa katika ziara ya siku tano ya kikazi mkoani Mwanza ambapo waziri Mkuu alisema.

“Mwanasheria utasimama kazi kuanzia leo na tuhuma zako zitachunguzwa kikamilifu na vyombo husika na uchunguzi ukibaini kama huna kosa utarudi kazini. hatutakuonea lakini hatuwezi kukuvumilia kwa utaratibu huo ulioufanya,” alisema Majaliwa.

Imeelezwa kuwa Novemba 2017 wakati alipokuwa anakaimu nafasi ya Ukurugenzi Mwanasheria huyo aliidhinisha malipo ya sh. milioni 279 zilipwe katika akaunti binafsi ya Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Antony Bahebe.

Kwa mujibu wa taarifa ya Waziri Mkuu Bahebe aliishtaki halmashauri hiyo akidai kulipwa fedha kwa ajili ya kazi ya ukandarasi wa mradi wa maji Igenge uliojengwa na kampuni ya ukandarasi ya Seekevim ambapo alisema  mradi huo ulianza 2014 na ulitakiwa ukamilike 2015,ambapo  Mwanasheria huyo aliidhinisha malipo hayo wakati ambao tayari hati maalumu ya uwakilishi ilikuwa imekwisha tangu Desemba 2015.

“Mwanasheria amemlipa Mwenyekiti wa Halmashauri kwa kufanya kazi na Halmashauri baada ya kuifikisha Halmashauri yake Mahakamani. Amemlipa fedha wakati kazi yenyewe ilikuwa haijaisha na aliharakisha malipo hayo kipindi ambacho Mkurugenzi hayupo, ”alisema Majaliwa huku  akiwakumbusha watumishi wa umma kuzingatia maadili ya utumishi na matakwa ya kisheria katika utekelezaji wa majukumu yao.

Akifafanua Majaliwa alisema fedha alizolipwa Bahebe zingeweza kutumika katika ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika halmashauri hiyo.

Katika ziara hiyo Waziri Mkuu alifungua mabweni ya watoto wenye mahitaji maalumu katika shule ya msingi ya Mitindo iliyoko wilayani Misungwi na pamoja na kukagua ujenzi wa vyumba vya madarasa.

Ukiacha na kipande hicho cha uozo uliofichwa,Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi imekuwa na historia mbaya kwa watendaji wa Wilaya hiyo kutafuna fedha za miradi mbalimbali ya maendeleo ambapo baadhi ya watendaji wa halmashauri hiyo wamekuwa wakibuni mbinu mbalimbali kuwahadaa wananchi.

Mwaka 2016 Kaimu Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Sanjo Charles Bulugu,alimchongea kwa Mkuu wa Wilaya ya Misungwi Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Eliud Mwaiteleke kwa kutoa taarifa za uongo katika mkutano wa Serikali ya Kijiji cha Sanjo akisema  kuwa,Mkurugenzi huyo alishindwa kufika katika mkutano wa kijijinihicho kwa kukosa gari la kumpeleka kusikiliza kero za wananchi hao.

Katika mkutano huo Bulugu alidai kuwa Mkuu wa Wilaya ya Misungwi alitoa agizo akimtaka Mkurugenzi kufika katika kijiji hicho kufuatia malalamiko yaliyotolewa na wananchi wa Kijiji cha Sanjo kwa kuuomba Uongozi wa Wilaya ya Misungwi ufike hapo kusikiliza kero zao.

Katika taarifa hiyo iliyotengenezwa ili kuwahadaa wananchi wa Kijiji cha Sanjo Bulugu alimsingizia Mkurugenzi wa Halmashauri ya Misungwi Eliud Mwaiteleke kuwa eti
amekwama kufika katika mkutano huo kutokana na kukosa usafiri kufuatia gari lake kuwepo katika usimamizi wa mitihani ya Taifa kwa wanafunzi wa Darasa la Saba.

“Ndugu zangu wananchi kwa niaba ya Mkurugenzi  napenda kuwaomba radhi kwa kuchelewa kufika hapa mgeni wetu sasa ni saa tano asubuhi ,ni kwamba mgeni wetu hataweza kufika kutokana na kukosa usafiri wa kumleta hapa,gari lake liko kwenye shughuli za Mitihani ya Darasa la saba”alisema Bulugu huku miguno na maswali toka kwa wananchi vikitawala.

“Hivi Mtendaji huoni kuwa huu ni uzembe wa makusudi,magari yote ya Halmashauri hayapo kweli? hata gari lake liko kwenye mitihani?mbona hawa watu wanataka kuturudisha tulikotoka? Sasa tunakuagiza Mtendaji ukamwambie Mkuu wa Wilaya kuwa agizo lake limepuuzwa! kwa nini Mkurugenzi asitumie hata Hiece?” alihoji mmoja wa wananchi waliokuwepo katika mkuitano huo.
Yaliyojiri baada ya Uchunguzi

Uchunguzi uliofanywa kipindi hicho Tanzania Daima lilibaini kuwa, taarifa hizo hazikuwa za kweli kwani Mkurugenzi huyo alikuwa safari ya kikazi Mjini Dodoma.
taarifa hiyo iliwakera wananchi na kuahidi kugomea mikutano ijayo iwapo hawatapata maelezo ya kutosha juu ya tukio hilo ambapo hadi leo hii wananchi hao hawajawahi kusikilizwa kutokana na kwamba mkutano huo ulikuwa kama kiini macho kuficha tuhuma zilizokuwepo kwa watumishi kipindi hicho.

Mwandishi wa Tanzania Daima alimtafuta Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi  ili kutolea ufafanuzi wa taarifa iliyotolewa na Afisa Mtendaji huyo ambapo Mkurugenzi alisema kuwa hazina ukweli.
“Mimi kwa sasa niko Mbeya,nimeshtushwa sana na taarifa hizo mimi nikose usafiri si ningeenda na pikipiki? Sisi kazi yetu ni moja tu nayo ni kuwatumikia wananchi na si vinginevyo sijui Mtendaji huyo kapata wapi maelekezo hayo ngoja nifuatilie”alisema Mwaiteleke.

Wakizungumza na Tanzania Daima kwa nyakati tofauti wananchi hao walisema kuwa wamekwazwa na kitendo cha Mkurugenzi kushindwa kufika kijijini jambo walilosema bila kumung’unya maneno kwamba ni uzembe.

Akiweka wazi siri zilizokuwa zimefichika katika maandalizi ya taarifa za uongo zilizotolewa na Kaimu Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Sanjo Mwenyekiti wa Kitongoji cha Nyasubi Meni Lutandula aliliambia Tanzania Daima  kuwa kuna udanganyifu mkubwa katika ujenzi wa tenki la maji katika kijiji cha Sanjo ambapo walibaini matumizi mabaya ya fedha za wananchi kiasi cha shilingi milioni 20,828,502;60 katika ujenzi wa mradi wa maji.

“Inasikitisha kuna ujenzi wa shule ambayo hata hivyo ilikuwa haijaanza kufanya kazi lakini tayari vyumba vimechakaa kutokana na kujengwa chini ya kiwango wananchi kulazimishwa kuchangia shilingi 6500 kila familia kwa ajiri ya ukarabati wa vyumba hivyo”.alisema Lutandula.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Sanjo Bukali John alipotakiwa kutolea ufafanuzi sakata la ujenzi wa madarasa chini ya kiwango alisema alikiri na kumuonya mwandishi asiripoti taarifa hizo.
“Nisingependa uendelee kufuatilia jambo hilo kwa kuwa wananchi tayari tumeshawashawishi wananchi na wamekubali kuchangia fedha kwa ajiri ya kurekebisha vyumba hivyo ni kweli kuna mapungufu yaliyojitokeza katika ujenzi wa vyumba hivyo lakini sitaki ufuatilie suala hilo maana tayari tumeshafanya vikao na wananchi na tumekubaliana wachangie fedha kiasi cha shilingi 6500 kila familia ili tuweze kukarabati vyumba hivyo” alisema Bukali.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Misungwi Juma Sweda alipotafutwa kuzungumzia kama alitoa agizo kwa Mkurugenzi ambapo alisema kuwa hana taarifa zozote juu ya agizo hilo na kwamba yeye hajawahi kufanya ziara katika kijiji cha Sanjo.
“Mimi sijawahi kufanya ziara yoyote katika kijiji hicho isipokuwa nilishiriki kikao cha Kamati ya Maendeleo ya Kata ya Fela hivyo sijui Afisa Mtendaji huyo alitoa wapi maelekezo hayo nitafuatilia kujua zaidi juu ya jambo hilo”alisema Sweda.
Baraza la Madiwani kuwapa Siku 30 kwa watendaji

Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi, limewapa muda wa siku 30 watendaji kushughulikia suala la makusanyo ya mapato ya ndani na utekelezaji wa mradi wa maji katika kijiji cha Fela uliokwama tangu 2013.

Azimio hilo lilipitishwa na baraza hilo wakati wa kikao kilichofanyika mjini Misungwi juzi, baada ya kubainika kuwa hadi Desemba 2017 halmashauri hiyo imekusanya Sh734.9 milioni pekee kati ya malengo ya kukusanya Sh2.06 bilioni.

Katika Baraza hilo Mbunge wa Misungwi, Charles Kitwanga aliwacharukia watendaji na kuwataka watoe  maelezo juu ya kusuasua kwa ukusanyaji mapato, hali inayokwamisha utekelezaji wa miradi.

Akitolea mfano wa kusuasua alisema kuwa katika mwalo huko Mbarika vitabu vya halmashauri vinaonyesha hakuna mapato yanayokusanywa, lakini hivi karibuni kamati ya uchumi na mipango ilipotembelea eneo hilo ilifanikiwa kukusanya Sh15,000 kwa muda mfupi, hali inayodhihirisha udhaifu katika ukusanyaji wa mapato.

Kuhusu mradi wa maji wa Fella ambao utekelezaji wake ulianza Juni 2013 na kutakiwa kukamilika Desemba mwaka huo, baraza limempa siku 30 mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Eliud Mwaiteleke kuhakikisha unakamilika na kutoa maji au uwekwe chini ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji.

Mradi huo ambao tayari umegharimu zaidi ya Sh644 milioni, unatarajiwa kunufaisha wakazi 6,473 wa vijiji vya Fella, Ngeleka na Bujingwa.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, mhandisi wa maji wa halmashauri hiyo, Ali Mruma alisema tayari maji yameanza kutoka na zinahitajika zaidi ya Sh3.8 milioni kununulia mashine ya kuyasukuma ili kuongeza usambazaji wa huduma kwa wananchi.

Diwani wa viti maalum, Christina Nyanda alisema maji hayo kata ya Mamaye yanatoka kwa kusuasua na kutaka wataalamu kutoa maelezo sahihi.

Mkandarasi wa kampuni ya COWI Tanzania Ltd inayotekeleza mradi huo, Ernest Tinka alikiri kuwapo upungufu na kuahidi kurekebishwa.

Siri zilizofichika nyuma ya miradi Misungwi.

1.      Kuna maslahi binafsi katika utekelezaji wa Miradi mbalimbali Wilayani Misungwi kutokana na baadhi ya viongozi wa Serikali na kisiasa kudaiwa kuwa ndiyo wamiliki wa makampuni yanayotekeleza miradi hiyo ambapo kwa haya aliyokutana nayo Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Suluhisho kuinusuru Miradi ya maendeleo dhidi ya Mchwa.
inatakiwa kuunda Tume Maalumu kwa ajiri ya kuchunguza ufujaji wa mali za Umma lakini pia watumishi wa Wilaya ya Misungwi wahamishwe kutokana na Mtandao wao unaokwamisha kujulikana kwa uozo kupitia kwa Kaimu Afisa Habari wa Wilaya ya Misungwi Thomas Lutego ambaye hata akiwa na shughuli hubagua Waandishi wa Habari kwa lengo la kuficha maovu hayo.
















Wednesday, February 14, 2018

Bundi atua Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu.

Na Antony Sollo Ushetu.
14.feb 2018

MGOGORO mkubwa umeibuka baina ya Emmanuel Makashi ambaye ni Diwani wa Kata na Christopher Rwagasanga Lyogelo ambaye ni Afisa Mtendaji wa Kata ya Sabasabini iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu Mkoni Shinyanga,hali iliyopelekea diwani huyo kuangua kilio katika kikao cha baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo akimtuhumu Afisa mtendaji huyokuhujumu shughuli za maendeleo ya Kata hiyo.

Akiwasilisha malalamiko yake mbele ya Madiwani hao kilichofanyika Februali 14 mwaka huu huko Ushetu Makashi lisema kuwa Afisa Mtendaji huyo amekuwa akibeza kila kitu kinachofanywa na Diwani huyo.

“Mheshimiwa mwenyekiti Afisa Mtendaji huyo amekuwa akichonganisha na wananchi huku akisema kwamba mimi sijasoma,na kuwaambia kuwa yeyendiye anafaa kuwa kiongozi wao akidai kuwa anashahada ya elimu ya juu na kuwaambia kwamba mimi sina uwezo wa kuwaletea maendeleo amekuwa akiwashawishi watendaji wa vijiji kutojishughulisha katika masuala mbalimbali ikiwemo uchangiaji wa shughuli za maendeleo”alisema Makashi.

Kutokana na uchungu aliokuwa nao Makashi aliangua kilio mbele ya viongozi mbalimbali waliohudhuria kikao cha baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo kilichoketi kwa lengo la kujadili mambo mbalimbali ya maendeleo ikiwamo miradi ya maendeleo kwa wananchi wa Ushetu.

Baraza hilo lilihudhuriwa na viongozi mbambli mbali wa Chama na serikali akiwemo mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga Mabala Mlolwa pamoja na katibu Tawala wa Wilaya ya Kahama, Timoth Ndanya ambapo Diwani huyo aliamua Mtendaji huyo kwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga huku akisema.

“Ndugu mwenyekiti kuna tatizo la kiutendaji katika Kata yangu ya Sabasabini kwamba, Afisa Mtendaji wa Kata amekuwa kikwazo kikubwa cha maendeleo kwa wananchi wangu, tangu aanze kazi kwenye Kata yangu mwaka 2016 hakuna maendeleo yoyote kwani amekuwa akiwagomesha wananchi kuchangia shughuli za maendeleo,” alilalamika Makashi.

Katika jitihada za kutatua mgogoro huo Makashi alimuomba Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Matomola Michael kufika katika Kata hiyo ili kuwapatanisha waendelee kuwatumikia wananchi huku akisema tangu kuanza kwa figisu figisu za Afisa Mtendaji huyo hadi sasa hakuna kitu kinachofanyika kutokana na mgogoro huo.

“Mheshimiwa mwenyekiti kibaya zaidi Afisa Mtendaji huyo amekuwa akiwashawishi na watendaji wengine wa vijiji wasinipe ushirikiano katika kutekeleza shughuli za maendeleo kwa wananchi kwa madai kwamba yeye ndiye kiongozi sahihi kutokana na kwamba ana nashahada ya elimu ya juu,kwa kweli nakuomba Mkurugenzi aunde tume ya uchunguzi dhidi yake,kama hutafanya hivyo tubadilishane ofisi wewe uwe diwani na mimi nikae kwenye kiti chako cha ukurugenzi ili na wewe uone vitendo ninavyofanyiwa na Mtendaji huyo,” alisema Makashi kwa uchungu.

Makashi alisema kuwa,kabla ya ujio wa Afisa Mtendaji huyo katika Kata ya sabasabini, kulikuwa na mahusiano mazuri na  wananchi kutokana na ushirikiano mzuri kati yake na kaimu afisa mtendaji aliyekuwapo kipindi cha 2013 /2015 kwa kufanikisha kutimiza agizo la Rais Magufuli juu ya kutengeneza Madawati mashuleni ambapo walifanikisha kuchonga madawati 74 yaliyogharimu kiasi cha shilingi milioni 8.8

Makashi alisema kuwa katika kipindi hicho alijitolea katika ujenzi wa matundu ya choo cha shule kwa kuchangia kiasi cha shilingi 150,000 na kuongeza kuwa kiasi cha shilingi milioni 5.3 kilitumika kujenga nyumba ya mganga  katika Zahanati ya Kata huku nguvu ya wananchi ni shilingi milioni 1.2.

Makashi alibainisha kuwa katika kipindi cha mwaka 2017 alifanikisha kujenga barabara ya Sabasabini kwenda Iponyang’holo kiwango cha changarawe yenye urefu wa kilometa 9 kwa gharama ya shilingi milioni 2.5 kwa ushirikiano na diwani wake wa viti maalum Felista Nyerere ambaye alichanga shilingi 300,000 kati ya fedha hizo,ambapo alidai kuwa tangu mtendaji huyo aanze kazi shughuli za maendeleo zimesimama kutokana na mgogoro wao.

“Mtendaji huyo alianza kazi katika kata hii tangu mwaka 2016, na alinikuta nikiwa vizuri na wananchi wangu  lakini tangu aanze kazi nimeshindwa kumuelewa labda anaitaka hii Kata!, maana kinachofanywa na Mtendaji huyu ni uvunjaji wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano na ninaona Mtendaji huyu anapingana na kasi ya Mheshimiwa Rais kwa kuamua kukwamisha shughuli za maendeleo kwa makusudi,mimi naomba Mkurugenzi aunde hiyo Tume ili kuweza kutatua mgogoro huu vinginevyo Kata hii haitaweza kupata maendeleo”alisema Makashi.

Akichangia hoja hiyo Diwani wa Kata ya Bulungwa Joseph Masaluta alilieleza baraza hilo kuwa wote wawili kwa maana ya Diwani pamoja na afisa mtendaji huyo wa Kata wapelekwe kwenye kamati ya maadili kwa lengo la kuhojiwa kwa kina ili kubaini chanzo cha mgogoro wao na kuongeza kuwa wawili hao wamekutana wote ni jeuri.
Katika majibu yake kwa diwani huyo Makamu mwenyekiti wa baraza hilo Gagi Lala ambaye ndiye alikuwa akiongoza baraza hilo alisema,

“Mkurugenzi haiwezekani mtu alalamike kiasi hiki tena hadharani inaonekana kuna tatizo linalopaswa kushughulikiwa, pamoja na kwamba kanuni za baraza haziruhusu kuingiza taarifa zilizo nje ya shughuli za baraza , mheshimiwa diwani ujumbe umefika kuwa mtulivu tutalishughulikia suala hili,” alisema Lala.

Kwa upande wake kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu Benjamin Onesmo ambaye pia ni afisa maendeleo ya jamii katika Halmashauri hiyo alisema kuwa kutokana na hali hiyo ofisi yake imelichukua suala hilo na italitafutia ufumbuzi wa haraka.
“Mheshimiwa Mwenyekiti ofisi yangu inalibeba suala hilo na litashughulikiwa na kupatiwa ufumbuzi wa Haraka,” alisema Onesmo”.

MWISHO.

                                                                                                          

Sunday, February 11, 2018

Afisa biashara Manispaa ya Ubungo awaliza mamilioni wafanyabiashara .

Na  Antony  Sollo Ubungo.

AFISA biashara wa Manispaa hiyo Geofry Mbwama anatuhumiwa kujipatia mamilioni ya fedha toka kwa wafanyabiashara wenye maduka pamoja na wajasiriamali katika manispaa hiyo baada ya kuingia kila duka akiomba Leseni ya biashara akiwa na Dereva wa Manispaa hiyo na kufanikiwa kujipatia kiasi kikubwa cha fedha akitumia nyaraka bandia za Serikali Tanzania Daima libaini.

Tukio hilo lilitokea desemba 13 mwaka jana katika Mtaa wa Mbezi Luis Manispaa ya Ubungo Jijini Dar Es Salaam ambapo Mbwama akiwa na gari la Manispa hiyo aliingia katika maduka na vibanda vya wafanyabiashara wadogo mafundi pikipiki hata wanaofanyia shughuli zao nje huku akihoji kama wana Leseni za biashara na pale ambapo alikuta hawana kwa sababu mbalimbali alifunga biashara na makufuli yake na baadaye aliandika nyaraka inayodaiwa kuwa ni feki na kuwapiga faini kati ya 321,000.

Akithibitisha kufanyiwa vitendo hivyo mmoja wa wajasiriamali (Fundi pikipiki) eneo la Mbezi makabe road Rahesh Shaban ambaye anajishughulisha na ufundi wa pikipiki alisema alilazimishwa kufunga shughuli zake baada ya kubainika kuwa hakuwa na leseni ya kufanya kazi ya ufundi licha  ya kujitetea kuwa alikuwa ameenda katika mamlaka ya Mapato Tanzania kwa ajili ya kupatiwa namba ya utambulisho wa mlipa Kodi ( TIN Number) lakini Afisabiashara huyo alimwandikia faini ya shilingi 321,000 na kumwamuru afunge shughuli zake.

“Mimi na wenzangu hapa tumemweleza kuwa tunazo baadhi ya nyaraka na kwamba tayari tulikuwa tumeshaanza mchakato wa kupatiwa namba ya utambulisho ya mlipa kodi( TIN Number) lakini hakutuelewa na matokeo yake aliandika faini katika nyaraka ambazo tunahisi ni feki kwa kuwa nyaraka yoyote ya Serikali huwa haiandikwi kitu chochote au namba ya mtu binafsi ambapo hata hivyo aliomba fedha kiasi kati ya 20,000, mpaka 60,000 tukampatia na hakutoa risiti yoyote”alisema Shabani.

Kwa kuwa Shaban aliona kuwa mahala pale ndipo anapopata riziki kwa ajili ya mahitaji ya familia yake,aliomba asamehewe lakini kilichoshangaza aliombwa shilingi 20,000 na Mbwama lakini hakupatiwa risiti jambo ambalo pia lilithibitishwa na wafanyabiashara wa duka la madawa yaliyoko jirani na Shabani ambao nao walitoa fedha kiasi cha shilingi 60,000 kila mmoja kutokana na kutishiwa kufungiwa maduka yao ambapo fedha hizo zilikabidhiwa kwa dereva wa Manispaa ambaye naye alikuwa akiwakaripia wafanyabiashara na kutoa vitisho vya kuwafungia biashara zao.

Tanzania Daima lilifuatilia nyendo za Mbwama na kukutana na malalamiko lukuki kwamba wafanyabiashara na wajasiriamali wa Mtaa wa Mbezi walio wengi walikuwa wameshachukuliwa fedha zao kutokana na tishio la kufungiwa biashara zao na Afisa biashara huyo akishirikiana na dereva wake.

Mwandishi wa gazeti la Tanzania Daima alimtafuta Mkurugenzi wa Manispaa ya Ubungo ambapo hata hivyo juhudi za kumpata Mkurugenzi huyo ziligonga mwamba kutokana na mwingiliano wa majukumu ambapo lilikutana na Katibu Tawala James Mkumbo ambaye baada ya kupatiwa taarifa juu ya kilichofanywa na watumishi hao dhidi ya wafanyabiashara nawajasiriamali na kuahidi kuzifanyia kazi tuhuma hizo ambapo tangu 13 desemba hadi leo hakuna taarifa zozote.

Mara kadhaa Mkumbo amekuwa akitakiwa kutolea ufafanuzi wa tatizo hilo lakini amekuwa akidai kuwa alikabidhi watu kufanyia kazi tuhuma hizo
“Kwa sasa niko Mwanza lakini kuna watu niliwapa jukumu la kushughulikia suala hilo lakini pia sisi hatufanyi kazi kwa pressure za waandishi wa Habari kwa sababu wanataka habari tukikamilisha utaratibu wetu tutafanya kinachostahili ”alijibu  Mkumbo kwa njia ya ujumbe wa simu ya mkononi.

Kinachoshangaza hapa ni kwamba hakuna taarifa zozote kuhusu ufuatiliaji wa tuhuma hizi pamoja na Katibu Tawala huyo kupelekewa Ofisini tuhuma zinazowakabili Afisa biashara wa Manispaa pamoja na dereva wa Manispaa ya Ubungo kwa takribani miezi miwili sasa jambo linalozua sintofahamu juu ya uadilifu wa watumishi hao

Wananchi waliozungumza na gazeti hili wameiomba Serikali kuwachunguza baadhi ya wafanyakazi wake hasa waliotumbuliwa kwa kuwa sasa wengi wako mtaani hawana kazi na wamegeuka Matapeli wanaotumia mbinu walizokuwa wamezizoea wakiwa kazini kutafuta fedha kwa njia za vitisho na inasemekana Mbwama na dereva wa Manispaa ya Ubungo kwa pamoja wamejipatia mamilioni kwa njia hiyo.

Mkurugenzi wa Manispaa ya Ubungo John Kayombo hakuwez kupatikana mara moja kuzungumzia tuhuma hizo ambapo juhudi za kumtafuta atolee ufafanuzi wa hatua gani zimechukuliwa dhidi ya tuhuma kwa watumishi hao kwa kukiuka maadili ya Utumishi wa Umma

MWISHO.






Friday, February 9, 2018

Wanaume waaswa kutojimilikisha maeneo ya familia



Na Antony Sollo


Februari 9,2018.

WANAUME katika  halmashauri ya mji wa Kahama Mkoani Shinyanga wametakiwa kuachana na dhana ya kujimilikisha  hati miliki za viwanja vyao, ili kutoa  kipaumbele kwa akinamama ili nao waweze kumiliki ardhi   hali ambayo itaepusha migogoro katika familia.

Akizungumza kabla ya kutambulisha mradi wa upimaji wa viwanja 4,000 katika kata ya Mhongolo  afisa ardhi wa halmashauri ya mji wa Kahama   Mashiri Magasa  alisema kuwa wanaume wilayani Kahama wamekuwa na tabia ya kujimilikisha maeneo yote yenye hati miliki  jambo ambalo siyo haki na kwamba hali kama hiyo pindi mwanaume anapofariki dunia humwacha mwanamke katika wakati mgumu.

Magasa  aliyasema hayo februari 8 mwaka huu wakati akizungumza na wananchi wa vitongoji vya sofi, bomani na Nyamhela vilivyoko katika Mtaa wa Mhongolo ambapo aliwaasa wanaume kuachana na dhana ya kujimilikisha maeneo ya familia kwani hali hiyo ndiyo chanzo cha mifarakano katika familia pindi baba wa familia anapoamua kuchukua hati hizo na kuomba mkopo katika taasisi za fedha na kushindwa kurejesha.

“Ifike wakati wanaume muwape fursa ya kumiliki ardhi wanawake kwani kufanya hivyo kunatoa usawa katika familia lakini pia kuna wakati mmoja wa familia hiyo akifariki hasa baba mwanamke hawezi kuhangaika kutokana kuwa tayari anakuwa ana mali halisi inayomfanya aendeleze familia, wanaume wakiachana na mfumo dume mwanamke akashirikishwa ipasavyo katika umiliki huo  hakutakuwepo na migogoro baina yao,” Alisema Magasa.

Katika hatua nyingine Afisa ardhi aliwataka wakazi wa mji wa Kahama kuhakikisha wanapima viwanja vyao kabla ya kufanya ujenzi au shughuli zozote za kimaendeleo na upimaji huo uende sambamba na utafutaji wa hati miliki ili kupunguza migogoro isiyokuwa na tija kwa jamii na kuwafanya waweze kukopesheka kirahisi katika taasisi za fedha.

“Kwa mujibu wa sheria ya Ardhi na mpango miji hakuna mwananchi yoyote hapa nchini anayeruhusiwa kufanya ujenzi wowote wa nyumba za makazi katika kiwanja chake bila ya kupimwa au kujenga nyumba bila ya kufuata ramani za mpango miji tukikuta unajenga kwenye eneo bila kibali tunasitisha ujenzi na kukupiga faini” alisema Magasa.

Kwa mujibu wa mpima ardhi  kutoka kampuni ya  Total Geo survey  Co.Ltd    Emmanuel William   ambaye anayeshughulikia upimaji wa viwanja katika kata hiyo alisema kuwa wananchi wanatakiwa kuchangia  gharama za upimaji ili kazi iweze kuendelea na kwamba mpaka sasa viwanja   4,000 vimepimwa na viwanja 1000 vimepitishwa na  wizara ya ardhi  Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa ajili ya kuwatafutia hati miliki wananchi.

Akizungumzia zoezi hilo William alisema kuwa lengo ni kupima viwanja 12,000 katika Kata hiyo na kuwataka wananchi kuongeza kasi ya kuchangia gharama ya upimaji ambayo ni shilingi elfu tisini 90,000 na kwamba gharama hiyo ni ndogo ukilinganisha na bei elekezi ya serikali ya kuanzia ambayo inaanzia shilingi laki tatu, 3,000,000. Kwa kila kiwanja.

Kwa upande wake Afisa Mtendaji wa mtaa wa Mhongolo  Denis  Diocles alisema kuwa lengo la kampuni hiyo ni kupima viwanja elfu 12, lakini viwanja vilivyofikiwa ni 4021, vilivyopewa namba ni 1335, ambavyo havijapewa namba ni 2686 na kutaja mradi wote unagharimu kiasi cha shilingi milioni 361 kati ya hivyo vilivyolipiwa ni 1192 na ambavyo havijalipiwa ni 2828.

Akizungumza katika zoezi la kutamburisha mradi huo Mwenyekiti wa mtaa wa Mhongolo Emmanuel Nangale alisema kuwa kukusanya shilingi milioni 361  kwa wakazi hao siyo kazi ndogo na kudai kuwa kiasi kilichokusanywa hadi sasa kinapswa kupongezwa licha ya watu kutohamasika kikamilifu na kwamba katika halmashauri hiyo ni Mtaa wa Mhongolo pekee umejitutumua katika zoezi hilo.

Mwisho.


Saturday, January 20, 2018

Kushamiri kwa Migogoro ya Ardhi Nchini



Makala:

Zikiwa zimepita siku chache tangu vikao vya Kamati za Bunge vianze mjini Dodoma hali ya mambo katika maeneo mbalimbali nchini si shwari kwani kumezuka mijadala mikubwa kutokana na madhira yaliyowapata wananchi kutokana na kupigwa,kuporwa mali ,kujeruhiwa kwa risasi za moto na Askari wakati wa utekelezaji wa operesheni za kuwaondoa wananchi wanaokaa katika maeneo yanayodaiwa kuwa ni Hifadhi pamoja na Ardhi inayodaiwa kutengwa kwa ajili ya Uwekezaji nk.

Vikao hivyo vilianza jumatatu ya tarehe 15 januari 2018,hii ikiwa ni kabla ya kuanza kwa Mkutano wa kumi wa Bunge,shughuli zilizopangwa kutekelezwa katika kipindi cha vikao hivi ni pamoja na ziara za ufuatiliaji ,uchambuzi wa miswada mbalimbali na kupokea maoni ya wadau pamoja na kupokea taarifa za utendaji za Wizara.

Kamati tatu za kisekta ambazo zitakuwa na jukumu la uchambuzi wa miswada mbalimbali ni pamoja na Kamati ya Sheria,Kamati ya Ardhi,Maliasili na Utalii pamoja na Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii.

Maoni yangu kwa wadau na wajumbe wa Kamati hizi watumie muda huu kuangalia namna ya kutatua tatizo lililomuelemea Mheshimiwa Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi  Wiliam Lukuvi ambaye kama angekuwa si Kiongozi Mahiri huenda Rais Magufuli angekuwa ameshamuweka pembeni kutokana na malalamiko likuki yanayoiandama Ofisi (Wizara)yake.

Kipekee niwapongeze Mawaziri hawa wawili Mheshimiwa Wiliam Lukuvi na Naibu wake Mheshimiwa Angelina Mabula kwa kazi kubwa wanayofanya ikiwemo kupokea na kufanyia kazi malalamiko takribani nchi nzima.

Ukweli Wizara hii ni ngumu,ina mianya mingi ya rushwa ambayo kama si umahiri wa Mawaziri hawa huenda Mahakama na Mabaraza ya ardhi kungefurika mafaili ya malalamiko zaidi ya haya,lakini kutokana na uchunguzi nilioufanya naona kabisa na ninaweka bayana kuwa Mawaziri hawa wamejitoa muhanga kwa ajili ya kupigania haki za wananchi wanyonge.


katika mkutano wa tisa wa bunge la kumi na moja November 16, 2017 akijibu maswali ya papo kwa papo Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhshimiwa Khasim Majaliwa aliulizwa maswali na wabunge Magdalena Sakaya (Kaliua) aliyetaka kujua Serikali imejipangaje kukabiliana na tatizo la mabadiliko ya tabia nchi suala ambalo ni la kidunia.

Katika majibu yake Waziri Mkuu alisema,
“Mheshimiwa Spika,mabadiliko ya tabia nchi yaliyokumba dunia na Tanzania ikiwemo,tunaendelea kukabili changamoto kwa  kuweka mipango mbalimbali kuhakikisha kuwa tunakabiliana na mabadiliko hayo,moja ya mikakati hiyo ni kusimamia Sheria ya uhifadhi wa Mazingira ili kuhakikisha Mazingira yanabaki yanasaidia kufanya mabadiliko ya hali ya hewa ya nchi yanabaki kuwa ya kawaida yanayowezesha binadamu au viumbe hai vyote ndani ya nchi kufanya kazi zake vizuri na kupata mahitaji yake vizuri”

Waziri Mkuu pia alisema kuwa Serikali imeendelea kusimamia Sheria za mazingira ambazo pia zinakinga maeneo mbalimbali hii ni pamoja na misitu,mito na maeneo mengine yote ili kukabiliana na hali hiyo.

Serikali pia imeendelea kutoa elimu kwa jamii kuwaelimisha Watanzania umuhimu wa Kutunza mazingira yetu kwa ujumla,zikiwemo taasisi za kimataifa zimeendelea pia kusaidia kupambana na tatizo hili.

Waziri Mkuu alitoa wito kwa watanzania nia wote kutunza mazingira na kwamba mabadiliko ya tabia nchi duniani hayatafanikiwa iwapo tutaendelea kuharibu misitu yetu,kuharibu vyanzo vyetu,tunaweza kukosa huduma za jamii zinazotokana na mabadiliko ya tabia nchi,hivyo ni muhimu sana kushirikiana na wataalamu kwa pamoja na wananchi wanaoishi na kila mmoja aliyepewa dhamana katika maeneo yao ili kuweza kushiriki kwa pamoja kuhifadhi Mazingira yetu.

Waziri Mkuu pia aliulizwa swali na Mheshimiwa Vedasto Edgar Ngombale (CUF) kuhusu shambulio lililofanywa julai 2017 na Askari Polisi ndani ya msikiti ambapo shambulio hilo lilipelekea kifo cha Shekh Ismail Weta na kuondolewa jicho kwa Shekh Abdalah Nakindabu ambapo Mbunge huyo alitaka kujua kama Serikali ina mpango wa kulipa fidia  kwa watu hao.

Akijibu swali hilo Mheshimiwa Waziri Mkuu alisema kuwa kwanza sina uhakika kama Askari walimshambulia mtajwa hapo na kumtoa jicho lakini jukumu la vyombo vya dola na Jeshi la Polisi likiwemo ni kulinda usalama wa raia na mali zao,si jukumu la polisi kwenda kumshambulia mtu na hatimaye Serikali ianze kufikiria kumlipa mtu fidia kutokana na shambulio lililofanywa na Askari Polisi na kama kuna Askari yeyote amefanya tendo hilo yeye mwenyewe nje ya majukumu yake ya kazi atachukuliwa hatua kama yeye aliyetenda kosa hilo.

“Serikali haiwajibiki kulipa fidia ikiwa si sehemu ya maagizo na wala si jukumu la majeshi ya vyombo vya dola bali ikithibitika mmoja kati ya watumishi wa vyombo vya dola ametenda kosa hilo na ikathibitika hivyo,yeye mwenyewe atawajibika kuchukuliwa hatua kali na ili kama kutakuwa na kulipa fidia itakuwa ni moja ya adhabu ambayo itatolewa na vyombo vinavyotoa hukumu”.alisisitiza Waziri Mkuu.

“Kwa hiyo Mheshimiwa Spika niseme tu kwamba,Serikali wala vyombo vyake vya dola havilengi kufanya kazi ya kuwatendea makosa wananchi bali ni kuwalinda wananchi pamoja na mali zao kama tulivyojipanga kufanya kazi”alisema Waziri Mkuu.

 Swali lingine ambalo nimelenga kulitumia kuthibitisha mambo yanayoashiria  kushamiri kwa migogoro ya Ardhi nchini liliulizwa mbele ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Ulyankulu Mheshimiwa Kadutu kuhusu kuzuiwa kwa wananchi kufanya shughuli za kilimo na ufugaji huku maeneo hayo yakiwa yamepimwa na vijiji vyake vimeandikishwa na wananchi wakiwa na (GN) Tangazo la Serikali.

Akijibu swali hilo Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano Khasim Majaliwa alisema nchi yetu ina mapori yaliyohifadhiwa kisheria,yana mipaka yake rasmi kwa mujibu wa Sheria zinazoyalinda,mapori haya yapo katika kila eneo,na ni budi kila mtanzania kushiriki kuyahifadhi,kumetokea uvamizi unaofanywa na waliojirani na maeneo hayo,ni kweli maeneo hayo yamekuwa na migogoro mingi kati ya mapori yetu na vijiji,kati ya mapori na wananchi ambao wanaoenda kufanya shughuli za kijamii huko ndani ambapo pia Serikali hairuhusu kufanyika kwa shughuli za kijamii.

Kutokana na migogoro hii ya muda mrefu,Waziri Mkuu alitoa agizo kwa Wizara ya Maliasili na Utalii kufanya mapitio ya mipaka na kuweka alama kwenye mipaka ya mapori yote.

Kilichobainika,Serikali ilikuwa imeshasajili vijiji hivyo na kulianza migogoro hiyo baada ya wataalamu walioanza kwenda kufanya kazi ya kubaini mipaka katika mapori hayo tuliwasihi wananchi walio kwenye vijiji vilivyo ndani ya mapori hayo wawaache wataalamu wafanye mapitio na waweke alama hizo zinazobainisha mipaka ya ramani baada ya hapo Serikali itakuja kuona ni kijiji gani kilicho ndani na je pale palipo kijiji malengo yetu ya uhifadhi yamefikiwa na bado ni Mahitaji sahihi ili baadaye tuje kufanya maamuzi ya au kupunguza maeneo ambayo kwa sasa kwa uhifadhi huo hauna tija ili kuondoa migogoro.

Waziri Mkuu alisema kuwa kazi hiyo inaendelea na aliagiza kuwa ifikapo tarehe 30 mwezi wa kumi na mbili 2017 wataalam hao wawe wamekamilisha kupima mapori ambayo bado  baada ya hapo Serikali iangalie ni vijiji vingapi vilisajiliwa na Serikali na viko ndani ya hifadhi/mapori hayo na kama vijiji hivyo bado viko kwenye maeneo yaliyo na tija kwa malengo ya uhifadhi au la ili Serikali itoe maamuzi mengine.

Waziri Mkuu alitoa wito kwa wananchi ambao wako kwenye hifadhi ambazo zimetambuliwa baada ya uwekaji wa alama uliofanywa na wataalam waendelee na kazi hiyo baada ya kazi hiyo Serikali ifanye mapitio na kufanya maamuzi kwa maslahi ya nchiikiwemo kufuta kijiji au kubadilisha mipaka ambapo mpaka hapo Mahusiano kati ya Serikali na wananchi yatakuwa yameenda vizuri na wananchi watashiriki kulinda mapori na hifadhi hizo.  
Nakubaliana na majibu ya Mheshimiwa Waziri Mkuu Khasim Majaliwa,sasa kero zilizoko katika maeneo mbalimbali Nchini ni namna wahusika walioagizwa kufanya kazi hiyo walivyogeuza zoezi hilo kuwa uwanja wa vita!

Iwapo Serikali imeweza kubaini mapungufu yaliyosababishwa na watendaji mbalimbali wa Serikali katika Taasisi zake kikiwemo Chuo Kikuu cha Dar Es salaam kuingia mikataba vivyo hivyo wapo watendaji wa Serikali walioamua kufanya wanayotaka katika agizo hili la Mheshimiwa Waziri Mkuu hivyo ,kamati ya Maliasili ifuatilie maeneo mbalimbali na maeneo ya kuanza nayo iwe ni Mikoa ya Tabora na Katavi ambapo mpaka hivi sasa vikao vya Kamati za Bunge vinavyoendelea vinaweza kuona ni jinsi gani watendaji wakiwemo wateule wa Mheshimiwa Rais walivyofanya unyama kwa wananchi wa maeneo hayo bila huruma kwa kuchoma vyakula,nyumba,na mali mbalimbali za wananchi jambo linalofanya wananchi waingie mgogoro na Serikali bila sababu.

Kuna aibu kubwa juu ya mambo waliyofanyiwa wananchi kwani wananchi wamefikia hatua za kutozwa fedha kiasi cha shilingi laki moja kabla hata ya utaratibu ulioelezewa vizuri na Mheshimiwa Waziri Mkuu ambapo ingefanyika hivyo,wananchi wasingeweza kupata madhara kiasi cha kusababishwa kwa vifo ,majeruhi,upotevu wa mali na kukosa makazi na aibu ni kwa vijiji vilivyosajiliwa.

Kwa kauli nzuri iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu ni kwamba atambue kuwa viongozi wa Serikali ngazi za chini wamekuwa wakifanya vitu vya kushangaza mpaka wananchi wanajiuliza wana haki gani kwa Serikali yao waliyoiweka madarakani ambapo baada ya muda imekuwa ikiwageuka na kuwaona hawana thamani.

Itambulike kwa ujumla wake kwamba katika zoezi la kuweka mipaka maeneo ya mapori hakukuwa na ushirikishwaji kwa wananchi katika mambo haya ikiwemo matumizi bora ya ardhi haukufanyika hivyo yote yaliyofanyika kuhusu utesaji,uporaji na mengine ilikuwa ni hulka kwa wateule wa Rais ambao walilewa madaraka na kuamua kufanya watakavyo jambo lililosababisha familia za wananchi katika maeneo mbalimbali nchini kuishi maisha magumu ikiwamo kutokuwa na makazi,huduma za kijamii nk.

Nashauri viongozi wakuu wa Kitaifa waweke utaratibu mzuri wa kufuatilia maagizo waliyotoa ili kuona utekelezaji maana pindi wanapoondoka katika maeneo hayo viongozi wa chini yao hugeuka miungu watu na kusahau maelekezo waliyopewa.

MWISHO.




Serikali Yapiga Marufuku Kulima Pamba kwa Mkataba



Zao la Pamba likiwa Shambani picha na Maktaba.
WAZIRI MKUU wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa amesema Serikali imekataza kilimo cha pamba cha mkataba kwa sababu kinawanyonya wakulima.
Waziri Mkuu ameyasema hayo jana (Ijumaa, Januari 19, 2018) wakati akizungumza na wananchi baada ya kukagua zahanati ya Hunyari wilayani Bunda, akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Mara.
“Ni marufuku kwa wanunuzi wa pamba kulima pamoja na wakulima kwa sababu wakulima wanakosa uamuzi wa kupanga bei. Kuanzia sasa zao hilo litauzwa kwa njia ya mnada.”
Alisema Serikali imeweka mkakati wa kuimarisha mazao makuu ya biashara ambayo uzalishaji wake umeanza kupungua likiwemo na zao la pamba.
Waziri Mkuu alisema Serikali imeamua kushiriki kikamilifu katika usimamizi wa kilimo cha zao la pamba kuanzia hatua za maandalizi ya shamba, pembejeo hadi masoko.
Pia Waziri Mkuu amewaagiza Maofisa Kilimo katika wilaya hiyo wawafuate wakulima vijijini kwa ajili ya kutoa elimu itakayowawezesha wakulima kulima kwa kufuata njia bora za kisasa.Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka wafugaji kuhakikisha wanakuwa na idadi ya mifugo kulingana na uwezo wa eneo lao.“Marufuku kulisha mifugo katika mashamba ya watu.”
Amesema Serikali itachukua hatua kali za kisheria kwa mfugaji yeyote atakayelisha mifugo yake katika mashamba ya wakulima kwani tabia hiyo huchangia migogo baina yao.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU
Source: MCHAMBUZI BLOG / 16 minutes ago



Friday, January 19, 2018

HABARI ZA KISIASA ZILIZOTIKISA MWAKA 2017 MKOA WA SHINYANGA


Na Antony Sollo Shinyanga.
Mbwembwe pamoja na ushangiliaji wa aina yake zilivyotawala katika Uchaguzi  ndani ya Chama cha Mapinduzi Mkoani Shinyanga kwa mwaka 2017.

Wahenga walishasema,ukitaka uhondo wa Ngoma ingia ucheze!!!!!!

Hivi ndivyo ilivyokuwa katika uwanja wa siasa ndani ya CCM Mkoani  Shinyanga  ambapo wanachama wa chama hicho walibuni mbinu ya kuhamasisha namna ya kumpata Mwenyekiti wa Chama hicho Mkoani humo ambapo ilikuwa ni burudani tosha kwa watazamaji wa Uchaguzi wakiwemo waandishi wa Habari.

Kabla ya Uchaguzi na hatua ya kutangaza matokeo ya Uchaguzi ndani ya CCM Mkoani shinyanga kuliibuka mbwembwe na ushangiliaji wa aina yake ambao hautakaa usahaulike.
Mmoja wanachama wa Chama cha Mapinduzi waliotia fola kwa mwaka 2017 ni Mheshimiwa Diwani wa Kata ya Kiloleli Manyama.
iliyoko Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga 

Diwani huyo  alijizolea umaarufu baada ya kubuni mbinu ya kupiga kampeni akitumia chupa ya chai (Thermos) ambayo ilikuwa imetundikwa katikamoja ya nguzo na kila aliyekuwa akipita aliitikisa na hata kuibusu kama ishara fulani kuonyesha dira na mwelekeo wa mgombea waliyekuwa wameona ataweza kuivusha CCM katika Uchaguzi 2020.

Mwandishi wa Makala hii alifuatilia nini ilikuwa uhalisia juu ya chupa ya chai iliyokuwa imetundikwa kama mtindo mpya wa upigaji kampeni ambapo kupata ufafanuzi huo mwandishi alimtafuta Diwani wa Kata ya Kiloleli ambaye alikuwa na haya ya kuzungumza.
Mwandishi: Mheshimiwa Diwani naomba kufahamu ni kipi kilichopelekea mtundike chupa ya chai katika moja ya nguzo za hema iliyokuwa ndani ya ukumbi wa kupigia kura.

Diwani: ndugu mwandishi,hii ni mbinu mpya tuliyoibuni baada ya kukutana na kukubaliana namna gani tutaweka ishara kwa ajili ya kusaidia upigaji wa kampeni kwa mtu wetu ambaye tunaamini anazo sifa za kuivusha CCM katika chaguzi zijazo ukiwemo wa 2020.
Mwandishi:Mbinu hii imebuniwa na nani?
Diwani: “Mbinu hii nimeiasisi mimi,si unajua siasa ni ushindani na siasa kwa upande mwingine ni ubunifu? Sisi kama wapiga kura baada ya kukaa na kuwapima wagombea wetu walioomba kupigiwa kura tuliona nani atakisaidia chama kukifikisha pale tunapotaka na hasa kwa kuendana na kasi ya Mheshimiwa Rais yaani HAPA KAZI TU”

Mwandishi: kwa hiyo mlikuwa mnapiga kura mkijua ni wapi na ni nani anayeshinda?
Diwani: Hapana! Kutokana na mfumo wa Demokrasia,kila mtu anayo haki ya kuchagua mtu au kiongozi anayemtaka hivyo baada ya kupiga kampeni nikiwapa wazo langu wanachama kwa ujumla wao,tulikubaliana kuwa kwa wale watakaokuwa tayari kuniunga mkono juu ya maoni na mawazo yangu ishara kubwa ni kufika na kuibusu na kuitikisa chupa hiyo na ndiyo kilichotokea na baada ya kuona watu wengi wakipita na kuibusu na kuitikisa chupa niliona wazo langu limekubalika na jambo hili lilinifanya nielewe kuwa kazi ya hamasa niliyoifanya ilikuwa imezaa matunda!

Kutokana na uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa makala hii, Diwani wa Kata ya Kiloleli Manyama ameweza kuwa mwanasiasa wa mwaka 2017 aliyebuni mbinu ya kuweza kupata matokeo ya kile alichokibuni na kushinda kabla ya kutangazwa kwa matokeo jambo ambalo wengi hata wale ambao wanaweza kuhonga ili wapigiwe kura imekuwa vigumu kujua nai kampigia kura na nani hakumpigia kura mpaka baada ya matokeo ndipo wanapokuja kupata matokeo.

Katika Uchaguzi huo uliofanyika Desemba 5, 2017 katika uwanja wa CCM Kambarage Mjini Shinyanga,Mabala Mlolwa aliibuka kidedea baada ya kuwabwaga washindani wake ambapo Mlolwa alipata kura 702  John Festo Makune kura 35 na Cornel Ngudungi  akiambulia kura 02.

Msimamizi wa uchaguzi na mlezi wa Chama hicho Mkoani Shinyanga Abdallah Juma Magodi  ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar alimtangaza Mabala Mlolwa kuwa ndiye mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Shinyanga.

“Naomba kusoma matokeo ya kazi tuliyoifanya,Ndugu Mabala Mlolwa kura 702  Ndugu John Festo Makune kura 35 na Cornel Ngudungi kura 02.
“Hivyo kwa mamlaka niliyopewa ya kuwa msimamizi wa Uchaguzi huu namtangaza ndugu Mabala Mlolwa kuwa ndiye Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Shinyanga.”alisema Abdallah.

Kwa nafasi ya mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa ikichukuliwa na Gaspar Kileo  aliyepata kura 702 dhidi ya wapinzani wake Bernad Shigela aliyepata  kura 33 na
Joyce Masunga-02.







  
Wajumbe wakiwa wanaendelea na zoezi la upigaji kura katika ukumbi wa Uwanja wa Kambarage Mkoani Shinyanga.Picha na Antony Sollo

 Diwani wa Kata ya Kiloleli Mh Manyama akiwa na Diwani wa Viti Maalumu pamoja na Mbunge wa Jimbo la Kishapu Mh Suleiman Nchambi mwenye fimbo wakijadili jambo wakiwa na chupa ya chai iliyokuwa ndiyo kivutio cha wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga wakiwa kwenye Uchaguzi wa chama hicho Uwanja wa Kambarage Mkoani Shinyanga. Picha na Antony Sollo.








Mwenyekiti wa  CCM Mkoa wa Shinyanga  Mabala Mlolwa akiomba kura kwa wajumbe ili wampigie kura  kwa nafasi aliyoomba kuwa Mwenyekiti wa Chama Mkoa wa Shinyanga:  Picha na Antony Sollo



Mjumbe wa NEC Mkoa wa Shinyanga Mh Gasper Kileo akiwa na wajumbe wa Chama Mkoa waShinyanga kabla ya kujiuzuru kwa ajili ya kufanyika kwa uchaguzi -  Picha na Antony Sollo 



 Wajumbe wa Mkutano Mkuu wakiendelea na zoezi la kupiga kura katika ukumbi wa Mkutano uliofanyika ndani ya uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga Picha na Antony Sollo

 Mh Manyama Diwani wa Kata ya Kiloleli akionyesha ishara ya kunywa maziwa ikiwa ni ishara ya ushindi baada ya kuasisi mbinu mpya ya upigaji wa kampeni mbinu iliyovutia wengi.


 Maballa Mlolwa akiwa na wagombea  wa nafasi mbalimbali kabla ya Uchaguzi wa nafasi ya Mwenyekiti ambapo aliibuka kidedea na kufanikiwa kuishikilia nafasi ya Mwenyekiti wa Mkoa wa Shinyanga Picha na Antony Sollo

Mwenyekiti wa  CCM Mkoa wa Shinyanga  Mabala Mlolwa akitoa neno la shukrani kwa wajumbe walimpigia kura baada ya kuibuka mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti wa Chama hicho Mkoani Shinyanaga:  Picha na Antony Sollo

MWISHO.

Kwa Taarifa Matukio mbalimbali pamoja na matangazo wasiliana na Katibu wa TAMRA kwa namba 0762 116 116/ 0762 117 117/ 0785 118 118.
antonysollo5@gmail.com